Wednesday, November 24, 2010

Watanzania wakiamua katiba mpya itapatikana -Odinga

Wakati msukumo wa madia ya kuwa na katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unaendelea hivi sasa hapa nchi, Waziri Mkuu wa Kenya, Raila Odinga amesema Tanzania haitakwepa kuwa na mabadiliko ya katiba iwapo wananchi watataka.

Hivi karibuni wabunge wa Chadema walitoka nje ya Ukumbi wa Bunge wakati Rais Jakaya Kikwete anajiandaa kutoa hotuba ya kufungua Bunge la Kumi, mjini Dodoma kwa madia kuwa hawatambui matokeo yaliyompa ushindi yaliyosababishwa na katiba mbaya.

Baada ya tukio hilo Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alitoa ufafanuzi kuwa wabunge wa Chadema walitoka bungeni kwa sababu katiba ya Tanzania inakasoro hivyo lengo lao ni kufikisha ujumbe kwamba wanataka mabadiliko ya katiba.

"Hatusemi hatumtambui Rais Jakaya Kikwete ila tumesema hatutambui matokeo ya uchaguzi wa rais na katiba iliyomweka madarakani ina kasoro nyingi kikiwemo kipengele kinachozuia kupinga matokeo ya rais mara baada ya kutangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi NEC," alisema Mbowe ambaye pia ni Kiongozi wa Kambi ya Upinzania bungeni.

Pamoja na kudai mabadiliko ya katiba, Chadema inataka Nec, iundwe upya kwa sababu iliyopo ambayo wajumbe wake huteuliwa na raisa haijaundwa katika mazingira ya kidemokrasia.

Raila alibainisha kuwa katiba nyingi za Afrika ikiwepo ya Kenya ambayo ilibadilishwa hivi karibuni zilipitwa na wakati kwa sababu ni za zamani.

Hata hivyo baadhi ya nchi za ukanda wa Afrika Mashariki na Kati ikiwemo Kenya zimefanya mabadiliko ya katiba na nyingine ziko kwenye mchakato kubadilisha.

Akizungumza juzi jijini Mwanza katika ziara yake ya siku moja ambayo ilikuwa maalum kwa ajili ya uzinduzi wa ndege aina ya Jet 5y-JL1 itakayo kuwa ikifanya safari zake mara tatu kwa wiki toka jijini Mwanza, Nairobi na Kisumu, Odinga alisema katiba ni hitaji la wananchi na iwapo wameanza kudai basi hakuna budi kuangaliwa kwa vile katiba ndiyo huchochea ustawi wa nchi.

Waziri Mkuu huyo wa Kenya alitumia fursa hiyo pia kuwapongeza viongozi waliochaguliwa na wananchi katika uchaguzi huo mkuu pamoja na kuipongeza Serikali ya Tanzania kwa kufanya uchaguzi wa amani bila ya kusababisha umwagaji wa damu.

Alisema kuwa Tanzania imeonyesha ukomavu wa siasa, imewahakikishia wananchi wake kuwa imekomaa kidemokrasia na imeonyesha mfano nzuri kwa nchi za Afrika Mashariki.

“Huu ni mfano mzuri sana katika Muungano wetu wa nchi za Afrika Mashariki zilizounda, ninawapongezeni sana kwa kuonyesha ukomavu wenu katika uchaguzi huu,” alisema Odiga.

Alisem yeye ni mwenyeji sananchini Tanzania na kufahamisha kuwa uwenyeji wake ulisababishwa na hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere.

Odinga alisema kwenye miaka ya 60 Serikali ya kikoloni nchini Kenya ilimnyima kibali cha kusafiria kwenda masomoni Ulaya.

Alifahamisha kuwa baada ya kunyimwa kibali Mwalimu Nyerere alimchukua na kumtunza nyumbani kwake kama mwanaye kisha alimtafutia kibali cha kusafiria kwenda Ulaya kusoma kwa miaka mitatu, hivyo kumfanya ajihisi kuwa yeye ni sehemu ya Watanzania.

Akizungumzia ufanyaji wa biashara halali katika mipaka ya Tanzania na Kenya Odinga, alisema kuwa Serikali za Tanzania na Kenya zinatakiwa kuwabana wafanyabiashara wanaofanya shughuli zao kupitia njia haramu kwa lengo la kujinufaisha wenyewe.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Abbas Kandoro alisema kuwa jitihada za kukomesha biashara hiyo haramu zinaendelea kufanywa na Serikali.

No comments:

Post a Comment